REST IN PEACE BRO......1980-2012
Kifo cha kiungo mshambulaji wa Simba raia wa Rwanda Patrick Mutesa Mafisango, kilichotokea usiku wa kuamkia jana majira ya saa 10 alfajiri, mazingira yake yalikuwa ya kusikitisha sana.
Akizungumzia mazingira ya ajali hiyo, rafiki wa marehemu aliyejitambulisha kwa jina la Olya Ilemba, ambaye alishuhudia kifo cha mchezaji huyo, alisema mauti ilimfika Mafisango wakati wakitokea kujirusha klabu ya Maisha, ambako bendi ya FM Akademia 'Wazee wa Ngwasuma' walikuwa wakipiga siku hiyo.
"Baada ya muziki kumalizika tuliondoka mimi Mafisango na watu wengine watatu, Mafisango ndiye alikuwa akiendesha gari aina ya Toyota Cresta nyeupe, lakini alikuwa akiendesha kwa mwendo wa kasi sana, tulipomuuliza akasema kuwa amechoka anahitaji kupumzika hivyo tumuache," alisema Olya.
Alisema walipofika maeneo ya VETA chuo cha ufundi Chang'ombe eneo ambalo unamalizikia ukuta, walikutana na mwendesha guta hivyo Mafisango akajaribu kumkwepa, lakini akiwa katika harakati hizo ghafla ilitokea pikipiki ambayo ilikuwa mwendo wa kasi sana.
Olya anasema wakati Mafisango anajaribu kumkwepa mwendesha Pikipiki bahati mbaya gari iliacha njia na kuparamia mtaro ambapo mbele yake kulikuwa na miti hivyo akaing'oa.
"Kwakweli ile ajali ilikuwa mbaya sana kwani baada ya gari kusimama tulimfuata Mafisango na kumkuta jicho la upande wa kushoto likiwa limechomoka huku akiwa ameumia vibaya kichwani, tukajaribu kuondoa kiwiliwili ambacho kilikuwa kimegandamizwa na usukani," alisema
Baada ya kumtoa hapo anasema kuna rafiki yao mwingine Gaspa Karemera alikuwa amechanganyikiwa baada ya kuhisi kuwa Mafisango amefariki, lakini alimwambia wajikaze ili wampeleke hospitali.
Anasema habati nzuri kuna teksi ilikuwa inapita hivyo wakaisimamisha na kumpakia mpaka hospitali ya taifa ya Muhimbili ambapo baadaye walithibitisha kifo chake.
Pia kiungo wa Yanga Haruna Niyonzima alisema kuwa msiba huo ni mzito sana kwa Mnyarwanda mwenzake, kwani jana saa ambayo Mafisango alipata ajali na kufariki ulikuwa muda wa yeye kuondoka kwenda Rwanda kujiunga na timu ya taifa ya Amavubi.
"Lakini cha kushangaza nilipoondoka nyumbani nilisahau tiketi ya ndege, ile na fika uwanja wa ndege nakumbuka kuwa sikubeba tiketi, wakati narudi nyumbani iliingia simu ya kunitaarifu msiba huo, kwakweli sikuamini mpaka pale nilipoenda Muhimbili," alisema Niyonzima.
Alisema kumbe zote hizo zilikuwa ni dalili kwani haikuwahi hata siku moja akasahau tiketi, lakini jana hali hiyo ilimkuta ambapo anasema siku moja kabla ya kifo chake walizungumza sana.
"Hakusita kunikumbusha kuwa, nitunze jezi yake namba 30 ambayo tulibadilishana wakati tulipocheza nao na sisi kufungwa mabao 5-0, aliniambia kuwa jezi hiyo nisiigawe kwa mtu yeyote kwani itakuwa ni kumbukumbu yangu, kumbe jamaa kama alijua anakufa, nitamkumbuka daima,"alisema Niyonzima
No comments